WADAU PANGANI WAKOMAA NA ELIMU!



Wadau mbali mbali wa elimu wilayani Pangani Mkoani Tanga wamesema wapo tayari kufikisha kwenye Jamii kile ambacho wamekipata kwa muda wa siku tatu mfululizo katika mafunzo ya Minna Dada yaliyomalizika mwishoni mwa wiki iliyopita katika kijiji cha Msaraza, ambapo mbali na mambo mengine suala la elimu lilijadiliwa kwa mapana zaidi.

Wakizungumza siku ya mwisho ya Mafunzo hayo wadau hao wamesema watahakikisha wanasimamia vyema maendeleo ya watoto shuleni, pamoja na kutumia Mafunzo hayo kujitoa katika mikwamo ambayo ilikuwa inawazuia kupiga hatua kwenye masuala ya maendeleo.

“Kwa sababu ilikuwa wengine ufahamu wetu ni mdogo na mpaka sasa hivi tumeelewa na elimu hii tutaipeleka kwa wenzetu na tutahakikisha wanaelewa na wanabadilika kama tulivyobadilika sisi, ili wao na sisi kwa kushirikiana tusongeshe mbele hili gurudumu la maendeleo”. Amesema mmoja ya wajumbe walioshiriki mafunzo hayo.


Kwa upande mwingine wanakamati hao wamesema wameweza kujitafakari na kuona makosa binafsi waliyowahi kuyafanya suala ambalo ni gumu, ila kupitia mafunzo hayo imekuwa rahisi kufanya hivyo, huku wakitoa shukrani zao za dhati kwa shirika la UZIKWASA kwa mafunzo ambayo yataendeleza kijiji chao.

 “Somo la kusema kuwa tujimulike wenyewe, hata katika dini ya kiislam tumeambiwa kuwa “sema kweli ijapokuwa inauma” ina maana mtu akubali kulitoa lake la moyoni ambalo linamkereketa hata kama ni uzembe aliusababisha yeye, akubali na akiri kwamba hili lilikwama kwa sababu yake yeye”. Amesema mmoja wa washiriki.


Mafunzo ya kambi ya Minna Dada yanatolewa na shirika la UZIKWASA, ambayo yana lengo la kujengeana uwezo na kuwezeshana wadau wa maendeleo na kamati ya shule za msingi namna ya kutumia mbinu wezeshi kutatua changamoto za wanafunzi shuleni na nje ya shule ili wafikie ndoto zao, mafunzo hayo pia yameshirikisha baadhi ya wataalamu kutoka halmashauri ya wilaya ya Pangani.



No comments

Powered by Blogger.