NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI JUMAA HAMIDU AWESO AFANYA ZIARA PANGANI





Naibu waziri wa maji na Umwagiliaji ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Pangani Mheshimiwa Jumaa Hamidu Aweso leo ameanza ziara katika jimbo lake kwa kukutana na Wazee na viongozi wa dini katika jimbo la Pangani kwa ajili ya kutoa shukurani zake pamoja na kujua changamoto zinazowakabili wazee hao.


 Akizungumza wakati  alipokutana na Wazee hao katika Ukumbi wa Halmashauri ya wilaya ya Pangani Mheshimiwa Naibu waziri amewaomba wazee hao kuwekeza kielimu kwa watoto wao  huku akimtaka Mkurugenzi wa halmashauri hiyo kuhakikisha wazee wanapata huduma za Afya  bure.
  






Kwa upande wao wazee waliohudhuria katika kikao hicho mbali na kumpongeza wamemuomba Naibu waziri huyo kutafuta mbinu mbalimbali kwa ajili ya kutumia maeneo  yenye fursa ya umwagiliaji pamoja na kutatua kero ya wafugaji kuingiza mifugo yao katika mashamba ya wakulima ili kuisaidia sekta ya kilimo kupiga hatua katika wilaya ya Pangani.



Pia Mkuu wa wilaya ya Pangani Bi Zainabu Abdallah Issa amemuomba Naibu waziri  huyo  kutumia fursa na ushawishi alionao sasa kwa ajili ya kufanikisha maendeleo katika jimbo hilo ikiwemo upatikanaji wa maji safi na barabara ya lami.



Hata hivyo Naibu waziri huyo amesema ameyapokea maombi hayo huku akisema tayari katika kipindi alichokuwa madarakani kama mbunge kuna mambo mbalimbali ya kimaendeleo anayahangaikia ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa meli ya kutoka Pangani Mpaka Zanzibar.



Hayo yanakuja ikiwa ni siku chache baada ya kuteuliwa na Mheshimiwa Rais kuwa Naibu waziri wa Maji na Umwagiliaji ambapo wazee mbalimbali katika jimbo la Pangani wamezungumzia kufurahishwa na hatua hiyo aliyoifikia.



No comments

Powered by Blogger.