FAHAMU YALIYOJIRI PANGANI WAKATI WA ZIARA YA MHESHIMIWA MWIGULU NCHEMBA



Serikali kupitia wizara ya mambo ya ndani ya nchi imejipanga kuhakikisha idara zote zilizopo chini ya wizara yake, zinazingatia maadili kwenye nafasi zao katika utekelezaji wa shughuli zake ili serikali iweze kufikia malengo yake.

Akizungumza katika studio za Pangani fm waziri mwenye dhamana kupitia wizara ya mambo ya ndani ya nchi Mheshimiwa Dk Mwigulu Lameck Nchemba, amesema kuwa mara zote serikali imejidhatiti katika kuhakikisha wizara zote zinawaletea manufaa wananchi wake, huku akipongeza serikali ya awamu ya tano kwa kutowafumbia macho watu kwenye jamii na hata watendaji wa serikali wanaobainika kwenda kinyume na matakwa ya serikali.

“Tumejidhatiti, utaweza kuona kwamba kwenye kila jambo ambalo serikali imeweka agenda yake maalum, pakitokea mtendaji hata raia akaenda kinyume na hayo amekuwa akifika katika mkono wa sheria, utaona kwenye vita ya madawa ya kulevya tumeweza kuchukua hatua na hii ni kwa sekta zote” Amesema Dk Nchemba na kuongeza kuwa.

“Hata wale ambao walikuwa kwenye vyombo vya haki na wakashindwa kutoa haki kwa kutokwenda na kasi ya vita ya madawa ya kulevya hata wenyewe walichukuliwa hatua, hata wachukuaji wa hatua ambao walistahili kuchukua hatua, pale palipoonekana hawakuchukua hatua, hatua zilichukuliwa dhidi yao. Kwa maana hiyo hakuna mchezo unaposikia hapa kazi ni kazi tu kweli kweli” Amesema Waziri wa mambo ya ndani Dk Nchemba.



Dk Nchemba ameongeza kuwa serikali ya awamu ya tano imetenda mengi mema katika mkoa wa Tanga kwa kuhakikisha inawapa viongozi vijana wenye kasi katika utendaji wao wa kazi kuanzia mkuu wa mkoa, wilaya na hata mbunge kwenye jimbo la pangani, na kuongeza kuwa ili halmashauri hiyo ipige hatua ni muhimu pia kuwatumia wafungwa katika shughuli za ujenzi wa taifa..

“Sehemu ya Magereza, wale waliopo kule tumesema tunawapeleka kwaajili ya urekebishwaji na kuna watu wako na vipaji vyao, ni faida na ni kitu chema kwa serikali kuhakikisha kwamba hawa watu hawatumii tu kodi za watanzania waliowema kuwalisha wao waliokuwa wamevunja sheria, kwa maana hiyo hili ni sharti kwamba lazima watumike kwenye shughuli za uzalishaji na si tu uzalishaji wa chakula, kuwatumia pia katika  shughuli nyingine za ujenzi wa taifa” Amesema Dk Mwigulu waziri wa mambo ya ndani.



Kwa upande wake Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mheshimiwa Jumaa Hamidu Aweso ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Pangani aliyeambatana na waziri Nchemba amesema kuwa, mara zote ataisemea Pangani hivyo katika suala la makazi bora kwa askari polisi jimboni mwake atachangia mifuko mia mbili ya Saruji.

Sisi kauli mbiu yetu, anayelala na mgonjwa ndie anayejua mihemo yake kwa hiyo aone hali halisi ya wafanyakazi wa jeshi la polisi. Unaweza ukawa baba wa watoto sita lakini siku ukatoka kazini ukaja na shati ukampa Saidi sio kama Abdalla na wengine sio watoto wako hapana. Tunajua majeshi yapo mengi sana lakini wa wilaya ya Pangani wanahitaji kusaidiwa, hata wagonjwa kuna wengine wapo hoi wanatakiwa wapelekwe sehemu ya dharura ICU”. Amesema Mh Aweso na kuongeza kuwa.

“Hata sisi Pangani tupo ICU tunakuomba angalia namna ya kutusaidia kituo hiki cha polisi na mimi kama mbunge kwenye mfuko wangu wa jimbo nitawapa mifuko 200 ya sementi kuchangia jitihada hizi katika kuhakikisha tunaboresha makazi ya askari”. Amesema Mh Jumaa Aweso Mbunge wa Jimbo la Pangani.



Naye Mkuu wa Wilaya ya Pangani Bi Zainab Abdallah Issa ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya Ulinzi na Usalama wilayani humo amesema kuwa, ujio wa Mheshimiwa Nchemba umekuja na mambo mengi hasa kuimarisha utendaji wa idara chini ya wizara yake, kwa kuhakikisha pia kunafanyika doria za mara kwa mara.

“Kwa kweli ni faraja kubwa kwa wanapangani, kwa sababu katika wizara ya mambo ya ndani kuna taasisi nyingi sana ambazo moja kwa moja zinaenda kuwagusa wananchi, pia nimshukuru kwa kutuletea gari kwa sababu jeshi letu la polisi tulikuwa na changamoto ya magari kwa hiyo kitendo cha wizara kutuletea gari maana yake kimeongeza ufanisi, usimamizi utaboreshwa na huduma zitaenda haraka kwa wananchi”. Amesema Mkuu huyo Bi Zainab.

Waziri wa mambo ya ndani ya nchi Mhe Mwigulu Lameck Nchemba amekuwa katika ziara fupi ya kikazi Wilayani Pangani kuanzia tarehe 4 hadi 5 February 2018, ambapo pamoja na shughuli nyingine pia amehudhuria uzinduzi wa kampeni za chama cha mapinduzi CCM huko katika kata ya Madanga.



No comments

Powered by Blogger.