PANGANI YAZINDUA RASMI WIKI YA MAJI DUNIANI LEO




Uzinduzi wa wiki ya maji kitaifa umetangazwa rasmi leo ambapo katika Wilaya ya Pangani imeelezwa kuwa juhudi za makusudi za utunzaji wa mazingira kwa ujumla, zinahitajika ili kufanikisha upatikanaji wa maji safi na salama hasa katika maeneo ya mjini na vijijini.

Akizungumza kwenye kipindi cha ASUBUHI YA LEO kinachorushwa na kituo hiki Mhandisi wa Maji kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Pangani Bwana Novat Wilson, amesema kuwa katika kuadhimisha wiki ya maji wamejipanga kutoa elimu kupitia kituo cha redio Pangani Fm ili kuikumbusha jamii jukumu lao katika kuhifadhi vyanzo vya maji.

“Ni vizuri kwamba leo kupitia Radio hii tuzungumze na wananchi katika maadhimisho haya ya wiki ya maji ambayo yapo kila mwaka mwezi machi tarehe 16 hadi 22, tunatoa elimu ya kuwakumbusha na kuwahamasisha wanajamii kujua wajibu gani wanapaswa kuchukua kuhusu uhifadhi na utunzaji wa vyanzo vya maji” Amesema Mhandisi Novat na kuongeza kuwa.


“Kwa wiki nzima kuna miradi tumepanga kuitembelea kuangalia inaendeleaje, ila pia kuendelea kuhamasisha wananchi kuhifadhi vyanzo vya maji wanavyovitumia. Na kuanzia kesho tarehe 17 ya mwezi huu wa Machi tutafika kijiji cha Mzambarauni ambacho mradi wake ulitekelezwa katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa maji safi vijijini, pia tutatembelea mradi wa maji wa Bweni ambapo tutakuwa na zoezi kama hilo, na tarehe 19 tutakuwa kijiji cha Mseko kwa sababu tumekuwa na changamoto ya maji kwa muda mrefu”Amesisitiza Bwana Novat.

Aidha Mhandisi huyo wa Maji amezungumzia hali ya upatikanaji wa maji safi na salama wilayani Pangani akisema bado kuna changamoto kutokana na miundombinu iliyopo kutoendana na uhalisia wa sasa, na kuongeza kuwa ili kulinda afya za watumiaji wa huduma hiyo ni muhimu kutibu maji hayo kuwa safi na salama kabla ya kuwafikia wananchi kwa ajili ya matumizi.



Kwa ujumla hali ya upatikanaji wa maji Pangani niseme ipo kati si chini sana wala si kwamba ipo juu sana, kwamba upande wa maji safi na salama tunachangamnoto, lazima tuwaambie watu kwamba tuna changamoto kwa sababu miradi mingine iliyofanyika zamani haikuzingatia zile standard za maji kwa sababu unakuta mradi umejengwa lakini una’Pump maji moja kwa moja kwenye mto unapeleka kwenye matumizi ya watu jambo ambalo sio zuri” Amesema Mhadisi wa maji Wilaya ya Pangani.

Na kusisitiza …. “Kwahiyo sasa serikali inachokifanya katika utekelezaji wa miradi ya maji safi na salama vijijini, kwamba watu inabidi wafahamishwe jinsi ya kutibu maji yaweze kuwa safi na salama kwa ajili ya matumizi kwa kuhakikisha kwanza yanachujwa na baada ya hapo yanatibiwa kabla ya kuingia kwenye matumizi”.

Mhandisi huyo wa maji Pangani, pia amekiri usugu wa changamoto za upatikanaji wa huduma hiyo katika baadhi ya vijiji wilayani humo ikiwemo kijiji cha Meka, Mseko na Masaika, na kusema kuwa mikakati yao ni kuhakikisha hadi kilele cha wiki ya maji Machi 22 mwaka huu wanawaacha salama wananchi hao wakipata maji ya uhakika kwa matumizi.

 (Watangazaji wa Pangani Fm kuanzia kushoto ni Hamisi Makungu pamoja na Kelvin Mpinga wakisikiliza kwa makini wakati wakifanya mahojiano na Mhandisi Novat Wilson katika studio za Pangani Fm kwenye kipindi cha Asubuhi Ya Leo)


“Ni kweli kwamba tumekuwa tunachangamoto ya maji katika baadhi ya miradi, kuna changamoto nyingine ambazo zimekuwa za muda mrefu lakini sisi tunakabiliananazo na zinaisha. Sasa kwa kijiji cha Mseko tunaimani kabla ya kilele cha wiki ya maji basi watakuwa wamerejeshewa maji angalau hii wiki inapoisha, wenyewe waseme kweli wiki ya maji imewaacha salama”. Amesema Bwana Novat Wilson.

Ameongeza kuwa.. “Kuhusu Masaika ni kijiji ambacho kilikuwa katika awamu ya kwanza ya kupatiwa miradi ya maji safi na salama vijijini ambayo ilianza mwaka 2006/2007, lakini shida iliyopo hapo ni kwamba visima vya pale kila kunapochimbwa maji hayapatikani kiasi cha kutosha kwa hiyo ule mradi haukuweza kukamilika kwenye awamu ya kwanza kutokana na kukosa chanzo cha maji cha chini ya ardhi.



Amesema… “Na katika wamu ya pili, pia tuliwachimbia kisima chenye urefu wa mita 100 ila pia kisima hicho kikawa na changamoto hiyo hiyo, kwa hiyo sasa njia mbadala ambayo tunaona inaweza ikafaa, ni kuwaweka kwenye mpango wa kuvuna maji kupitia mabwawa yaliyopo pale ambayo tukiyaboresha vizuri, yale maji tukiyachuja na kuyatibu yanaweza yakawa maji mazuri tu kwao” Amesema Mhandisi huyo.  

Maadhimisho ya Wiki ya Maji kitaifa na kimataifa yanayofanyika kila mwaka ifikapo tarehe 16 hadi 22, na mwaka huu wa 2018 yamebeba kauli mbiu isemayo “Hifadhi maji na Mfumo wa Ikolojia kwa maendeleo ya Jamii”, ambapo kwa wilaya ya Pangani kilele cha maadhimisho hayo yanatarajiwa kufanyika katika kijiji cha Boza Wilayani humo.


No comments

Powered by Blogger.