CHANGAMOTO YA MAJI BADO KITENDAWILI KWA WAKAZI WA MASAIKA WILAYANI PANGANI


Wananchi wa kata ya Masaika wilayani Pangani wameiomba serikali hususani halmashauri ya wilaya kuweka jitihada katika ufanikishaji na upatikanaji wa maji safi na salama kutokana na adha wanayokutana nayo kwa sasa.

Wakizungumza na Pangani Fm baadhi ya wananchi wa kijiji cha Masaika Mlimani wamesema kuwa hali ya upatikanaji wa maji katika eneo lao sio nzuri kutokana na kisima kilichokuwepo hakikidhi huduma ya maji kwa kila kaya jambo linalowalazimu kujiwekea idadi ya ndoo tatu kwa kila nyumba.

“Masaika bado suala la maji linasumbua ni gumu pamoja na jitihada zinazofanyika za uchimbaji wa visima lakini bado visima hatujafikia kuwa navyo kabisa, na tunatafuta maji kwa foleni, mtu unaamka kuanzia saa kumi za usiku na kurudi nyumbani saa mbili au saa tatu asubuhi, kwa kweli sisi kina mama tunapata shida sana.’’ Amesema mama mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Hidaya.

Bi Amina Awadhi ni mjumbe aliyechaguliwa na kamati ya kusimamia uchimbaji wa visima vya maji katoka katika kijiji cha Masaika Mlimani kwa upande wa wananchi, ametumia nafasi hii kuwaomba wataalamu wa maji na wachimbaji visima katika kata ya Masaika kuzingatia kukutana na wenyeji kabla ya utafiti wa uchimbaji.

 “Mimi kama mmoja kati ya wananchi niliyechaguliwa na kamati, niwaombe serikali pamoja na injinia wa maji kipindi watakachokuja Masaika kutuchimbia visima ni vyema wakakutana na wenyeji wa hapa ili tuwaonyeshe sehemu sahihi ambayo watapata maji’’ Bi Amina.



Bwana Michael Richard nae ni afisa mtendaji wa kata ya Masaika, amesema kwa sasa mpango uliopo kwa wanakijiji wa eneo hilo ni kuzifufua sehemu ambazo zina uwezekano wa kupata maji ili kuleta nafuu kwa wananchi hao.

‘’Mpango wetu kama kijiji ni kuzifufua sehemu ambazo zina uwezekano wa kupata maji na kuna bomba pia tutalifufua, wakazi wa Masaika wanapata shida na hata maji wanayoyatumia ni ya Bwawa na hutumiwa sana na wanyama hivyo si safi na salama’’ Amesema Bwana Michael.

Kwa upande wake Mhandisi wa maji kutoka halmashauri ya wilaya ya Pangani Bwana Novat Wilson amekiri kuwepo kwa changamoto ya upatikanaji wa maji eneo la Masaika, huku akieleza mpango mkakati uliopo wa kufanya utafiti utakaopelekea kuweka miundombinu mizuri ya upatikanaji wa maji safi na salama.

“Mipango yetu kama serikali ni kulifanyia matengenezo Bwawa lililopo hepo eneo la Masaika na tutalitumia katika uvunaji wa maji ya mvua na naamini tukiliwekea miundombinu mizuri wananchi watanufaika na Bwawa hilo’’ Amesema Mhandisi wa maji Bwana Novat.

Ameongeza kuwa…‘’Matarajio yetu kwa Masaika baada ya zoezi la usanifu wa hilo Bwawa tumeziweka katika mikakati ya mwaka wa fedha 2018/2019 kwa hiyo tumeiweka bajeti hiyo ili ifikapo mwezi wa sita mwaka huu huenda tukapata hizo fedha kwa ajili ya matengenezo.

No comments

Powered by Blogger.