"WANAWAKE PANGANI HAKUNA KUKATA TAMAA"- AFISA UTUMISHI


Wanawake wilayani Pangani wametakiwa kutokata tamaa katika utafutaji wa kipato ili kujiletea maendeleo yao na taifa kwa ujumla.

Hayo yamezungumzwa na Afisa Utumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Pangani Bi Mwanaidi Nondo wakati akizungumza na Pangani Fm ofisini kwake na kuongeza kuwa mwanamke akikata tamaa hawezi kufika mbali hivyo amewasihi kujituma kwa bidii ili kuiletea jamii mabadiliko.

‘’Mimi nawashauri wakina mama wenzangu tusikate tamaa kwa sababu unapojikatia tamaa mwenyewe huwezi kufika mbali, kweli tuna changamoto nyingi tunazozipata kwenye utendaji wa kazi mambo ya biashara na kifamilia yaani kikubwa ni kutokukata tamaa, tujipe moyo, kwani nina imani kuwa wanawake tunaweza kama tukijiamini basi tutafika mbali.’’ amesema Bi Mwanaidi.

Amesema Halmashauri ya Pangani imejipanga vizuri kuadhimisha siku ya wanawake duniani ambapo kiwilaya itakayofanyika kijiji cha BOZA kata ya KIMANG’A na kuwasihi wanawake kujitokeza kwa wingi katika sherehe hizo.

’Kama halmashauri tumejipanga vizuri kuadhimisha siku ya wanawake duniani inayotarajiwa kufanyika tarehe 8/3/2019 na tumejipanga vizuri na tumetoa ushirikiano mkubwa sana ili tufikie malengo ya siku hii, hivyo nawashauri kina mama tujitokeze kwa wingi ili tubadilishane uzoefu’’ amesema Bi Mwanaidi.

Kauli mbiu ya mwaka huu 2019 ya maadhimisho ya siku ya mwanamke duniani inasema kuwa “badili fikra kufikia usawa wa kijinsi kwa maendeleo endelevu”.

No comments

Powered by Blogger.