MHESHIMIWA AWESSO AISHUKIA MAMLAKA YA MAJI PANGANI MJINI, AIPA MASAA 24 MAJI YAPATIKANE



Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji nchini Mheshimiwa Jumaa Hamidu Awesso ameitaka Mamlaka ya Maji Pangani Mjini (PAWASA), kuhakikisha hadi kufikia kesho tarehe 05/12/2017, hali ya upatikanaji wa maji inatengemaa katika eneo la Pangani Mjini kabla ya hatua za kinidhamu kuchukuliwa.

Akizungumza na Pangani Fm kwa njia ya simu mapema leo, Naibu Waziri huyo ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Pangani amesema kuwa, amepata taarifa kuwa hali ya upatikanaji wa Maji Pangani Mjini sio wa kuridhisha, hivyo kuitaka Mamlaka husika kuchukua hatua haraka.

“Nimepata taarifa kuwa hapo Pangani Mjini leo ni siku ya tatu au ya nne maji hakuna kabisa, na hakuna taarifa yoyote, sasa nataka niwaombe mamlaka ya maji Pangani Mjini, wahakikishe maji yanapatikana kesho, ili wananchi wapate maji, kama kuna kikwazo chochote watoe taarfa mapema kabla hatujaanza kuchua hatua kwa watendaji wakuu” alisema Mheshimiwa Awesso.

Hivi karibuni Mamlaka ya Maji Pangani Mjini kupitia kaimu meneja wake Bwana John Kisiwa, iliwaomba radhi wateja wake kufuatia kuharibika kwa mashine ya kupandishia maji iliyopo eneo la Boza, Mheshimiwa Naibu Waziri akatoa wito kwa Mamlaka hiyo kufuatia kuharibika kwa mashine hiyo
“Mashine hata kama imeharibika inatakiwa kurekebishwa kwa wakati ili wananchi wapate maji kwa maana wao hawafahamu, kwa hiyo ninachotaka mamlaka itimize wajibu wao ili kutatua tatizo hilo, wafanye kazi usiku na mchana ikiwezekana, lakini waone umuhimu wao kwa jamii” alisema Mheshimiwa Naibu Waziri.

Katika hatua nyengine Mheshimiwa Jumaa Awesso ameweka bayana adhma ya serikali katika kuboresha huduma ya upatikanaji maji katika maeneo ya Mbugani, Langoni pamoja na eneo la Masaika, huku akiwataka wataalamu kutoka Halmashauri ya Pangani kuwashirikisha wananchi wa maeneo hayo ili kujua vyavyo sahihi vya upatikanaji maji.

“Sasa hivi visima tutakavyochimba ni eneo la Mbugani, Langoni lakini wananchi wetu wa Masaika wamekuwa na tatizo kubwa la maji, wataalamu walichimba kwa mara ya kwanza lakini hawakufanikiwa, lakini sasa niwaombe wataalamu wa Halmshauri wawashirikishe awamu hii wakienda kuchimba basi wawashirikishe wananchi wa Masaika katika kutambua vyanzo sahihi vya maji” Alisema Mheshimiwa Jumaa Awesso.

Mheshimiwa Jumaa Awesso ambaye anatarajiwa kufanya ziara ya kikazi mkoani Singida hivi karibuni, amewaomba wananchi wilayani humo kutunza vyanzo vya maji kwa lengo la kutokukwamisha huduma hiyo muhimu kwa maisha ya binadamu.

No comments

Powered by Blogger.