HATIMAE KITUO KIMOJA CHA MAFUTA PANGANI CHAANZA KUFANYA KAZI



Siku tano baada ya Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA mkoa wa tanga kuvifungia vituo viwili vya Mafuta mjini Pangani kwa kosa la kutotumia mashine za kutolea risiti za EFDs hatimaye leo kituo kimoja cha Mafuta cha TOC mjini humo kimeanza kutoa huduma baada ya kufunga mashine hizo.

Akizungumza na Pangani fm Mkurugenzi wa kituo hicho Bwana Swaleh Amar Abdallah amesema baada ya  kufungiwa kutotoa huduma waliwaita mafundi wanaohusika na ufungaji wa mashine hizo za EFDs na Mapema leo Januari 10, 2018 wameanza kutoa huduma kama kawaida.



“Huduma tumeianza siku ya leo saa tatu asubuhi na ilisitishwa na TRA kwa sababu ya kutofunga mashine za EFDs lakini tumejitahidi kadri ya uwezo wetu kurekebisha hilo tatizo tumewaita mafundi kutoka Tanga na Dar es Salam kwa hiyo walikuja hapa Pangani kukaa kwa muda kama siku mbili hivi, tunashukuru Mungu hapa kila kitu kipo vizuri na huduma ipo masaa 24” Amesema Bwasema na Swaleh ambaye mkurugenzi wa kituo hicho.

Mbali na kuelezea walivyoathirika baada ya kufungiwa kutotoa huduma hiyo Bwana Swaleh amesema tangu asubuhi walipoanza kuzitumia mashine hizo za EFD  hakujajitokeza changamoto yoyote ya kiufundi kupitia mashine hizo.

“Kutuathiri kweli imetuathiri kwa sababu tuna wateja wetu wengine kutoka Kipumbwi huko kwa hiyo unakuta yani akija mpaka hapa halafu akakosa huduma ya mafuta yani hajisikii vizuri anatuona kama ni uzembe wa kazi, kusema kweli maendeleo ni mazuri na bado hatujaona changamoto yoyote kwa sababu hizi kadi tulizoweka ni mpya na hii mashine tuliyofunga ni mpya umeona kwa hiyo hatujapata changamoto yoyote” Amesema Bwana Swaleh Abdallah.



Kwa upande wao wateja wa mafuta katika kituo hicho wameelezea kufurahishwa na kurejea kwa huduma ya mafuta wakisema kituo hicho kilipofungiwa walipata adha kubwa ya kufuata huduma hiyo wilaya jirani ya Muheza na kusababisha waendashaji wa vyombo vya moto hususan pikipiki kulazimika kununua bidhaa hiyo kwa bei ya juu.

“Tumefurahi sana kupata huduma hii ya mafuta, walipofungiwa tulipata shida sana kwa sababu tulikuwa tuna nunua mafuta kwa shilingi elfu tatu ambayo ilikuwa inatugharimu sana”. Amesema mmoja wa waendesha pikipiki mjini Pangani.

Kituo cha TOC ni miongoni mwa vituo viwili vya mafuta hapa mjini Pangani vilivyofungiwa na mamlaka ya Mapato Tanzania mnamo tarehe 5 Januari mwaka huu kwa kosa la kutotumia mashine za kielektroniki za EFDs.

No comments

Powered by Blogger.