PANGANI MASHARAKI YAPIGA MARUFUKU KUPOKEA WAGENI BILA YA KUTOA TAARIFA



Wananchi katika kijiji cha Pangani Mashariki Wilayani Pangani, wameonywa kuendelea kupokea wageni bila kuwatolea taarifa zao kwa uongozi wa kijiji, na kwamba yeyote atakayebainika kufanya hivyo atachukuliwa hatua kali za kisheria

Akizungumza na Pangani fm Mwenyekiti wa Kitongoji cha Funguni kata ya Pangani Mashariki wilayani humo Bwana Salimu Hatibu Kiraba, amesema kuwa wananchi katika kata hiyo wamekuwa na tabia ya kupokea wageni kienyeji kiasi cha kusababisha maafa katika jamii, hivyo pindi msako utakapofanyika mwenyeji na mgeni wake wote watakamatwa.

Bwana Kiraba ameongeza kuwa wananchi kutoa taarifa kwa uongozi pindi wanapopata wageni sio ombi, bali ni agizo lililopo kisheria hivyo amewataka waache mazoea kwani ni lazima utaratibu huo ufuatwe.
‘’Tuna tabia ya kuwapokea watu kutoka maeneo mbali mbali wakiingia katika majumba yetu kama vile wanafamilia tunawaomba kwamba taarifa zipatikane kwenye viongozi  na wenyeviti wa vitongoji kwa sababu unapompokea mtu kinyume na utaratibu atakuja kukamatwa kwa sababu serikali haimtambua’’ amesema Kiraba.

Aidha Bwana Kiraba amesema utaratibu huo hauangalii ndugu, jamaa wala rafiki, na taarifa zinatakiwa zitolewe hata kwa mgeni anayelala usiku mmoja ili kuepusha usumbufu iwapo madhara yatatokea.



‘’sio wiki hata kama kaja na kalala asubuhi akafanya safari unatakiwa kumtolea taarifa kwa sababu ni binadamu  awe ndugu awe nani, binadamu anatembea na umauti, hata kama ni baba yako unatakiwa umtolee taaarifa, akifariki nyumbani kwako tutakushughulisha wewe’’. Amesema Kiraba.

Bwana Salimu Kiraba amesema jambo hilo mara kwa mara wamekuwa wakilikemea lakini jamii imekuwa ikipuuza matamko kama hayo pindi wanapoyatoa, hivyo kwasasa kumekuwa na matukio mbalimbali ikiwemo wizi uliovuka mipaka.

‘’hii hali tunaizungumzia sana lakini watu wanapuuza na sasa hivi kuna wizi wa reja reja na hata kama tunasema huu wizi ni wa kawaida lakini chanzo wanaotuathiri  ni wageni wanaoshirikiana na vijana wetu na kama kukatokea mgeni kaiba ni lazima kumkamata kama ameripotiwa.’’ Amemalizia Kiraba.

Hatua hii, ni sehemu ya jitihada za kudumisha hali ya ulinzi na usalama Wilayani Pangani, hasa kuhakikisha wageni wote wanatambulika kila wanapofika ili wasivunje sheria za nchi.

No comments

Powered by Blogger.