JESHI LA POLISI PANGANI LASISITIZA AMANI NA USALAMA KAMPENI ZA UDIWANI KATA YA MADANGA



Jeshi la polisi wilayani Pangani limesema kuwa halitamvumilia mtu yeyote mwenye nia ya kuvuruga kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani, unaondelea katika kata ya Madanga wilayani humo.

Akizungumza na Pangani Fm, kamanda wa polisi wilayani Pangani Bi Christina Musyani amesema kuwa, mbali na kubaini makundi yanayotaka kuwatisha wanawake wasiende kupiga kura, pia amesisitiza suala la amani na usalama wakati wote wa kampeni, huku jeshi la polisi likijipanga kushiriki katika kila mkutano.

“Yako makundi yanataka kuwatisha wanawake wasije kujitokeza kwenda kupiga kura! Hapana, uchaguzi ni uhuru na ni demokrasia ya kila mmoja, kila mmoja anatakiwa kutumia nafasi hii kwaajili ya kumchagua yule anayemtaka na anadhani kwamba atasaidia katika kuleta maendeleo yake na atafurahia uongozi wa kiongozi huyo”. Amesema hivyo Kamanda Musyani na kuongeza kuwa…..

“Kila ambapo kuna ratiba kutakuwa na mikutano tutakuwepo, kuhakikisha kampeni zinakwenda salama” Amesema Kamanda Christina Musyani

Kamanda Musyani pia amewataka wagombea wanaowania nafasi ya udiwani katika kata hiyo, kunadi sera zao kwa kufuata utaratibu pamoja na miongozo ya kampeni iliyowekwa ili kujiepusha na uvunjifu wa amani pamoja na kulinda misingi ya demokrasia iliyopo hapa nchini.

“Kila anaeuza sera, auze huku akiangalia miongozo ya kampeni ikoje mpaka uchaguzi, aangalie pia je sheria zikoje, kwa hiyo tutumie nafasi yetu, ni uhuru wetu, demokrasia yetu lakini isilete madhara, kila mwenye kampeni afanye kwa usalama na amani na hatimaye tujetufike uchaguzi na hata baada ya uchaguzi tuendelee kudumisha amani yetu na ushirikiano wa kuijenga Pangani yetu. Amese kwa msisitiza Kamanda Musyan.



Kwa upande mwengine Kamanda Musyani hakusita kuwashauri wananchi wa Madanga kujiepusha na kampeni za ushawishi na mihemko kutoka nje ya eneo lao, kwa kuwa wao ndio wanaojua hali halisi na diwani wanayemtaka ambaye atakuja kushirikiana na madiwani wengine kwa lengo la kuiletea Pangani maendeleo.

“Huu ni uchaguzi mdogo wa ndani ya kata kwaajili ya kumtafuta diwani wa Madanga, kwa maana hiyo hatutarajii kwamba ushawishi mkubwa utoke nje, ni wanaMadanga ndio ambao wanafahamu hali halisi iko vipi, ukiacha wanaMadanga pia kuna wanaPangani kwahiyo hatutarajii kwamba ushawishi utoke nje, vurugu zije kutoka nje, sisi tunafahamiana wanaPangani na  tunajua kwamba tukipata kiongozi bora Madanga basi Pangani itasonga mbele kwa sababu atashirikiana na madiwani wenzake, lugha itakuwa moja, Pangani itaenda mbele”. Amesema Kamanda wa Polisi (W) Pangani Christina Musyan.

Kampeni za uchaguzi mdogo katika kata ya Madanga zilizinduliwa rasmi na mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya hiyo Bwana Sabas Damian Chambasi mnamo tarehe 21 January 2018, ambapo zoezi la upigaji kura linatarajiwa kufanyika tarehe 17 mwezi wa pili mwaka huu.

No comments

Powered by Blogger.