WAMILIKI WA MASHINE ZA KUSAGA NA KUKOBOA WILAYANI PANGANI WATAKIWA KUFUATA UTARATIBU



Baadhi ya wakazi wilayani Pangani wamewalalamikia wamiliki wa mashine za kusaga na kukoboa Mahindi kwa kutojali muda wa kufanyakazi hali ambayo inaleta kero kutokana na kelele zinazotokana na mashine hizo hasa nyakati za usiku.

Wakizungumza na Pangani Fm baadhi ya majirani walio karibu na mashine hizo wameeleza kuwa mashine hizo zilizopo maeneo ya makazi yao, hufanya kazi hadi saa nne au saa sita usiku, hali ambayo inawafanya washindwe kupumzika.

Mbali na kelele, pia wananchi hao wameongeza kuwa, uwepo wa mashine hizo katikati ya makazi ya watu umekuwa ni kero kutokana na nguvu za mashine hizo zinazotoa mtikisiko unaosababisha nyumba zao kuota nyufa.



Kwa upande wake Afisa Mazingira wa wilaya Pangani Bwana DAUDI MLAHAGWA amesema kuwa kwa mujibu wa sheria ya viwanda vidogo kama mashine ya kusagia Mahindi pia ipo kwenye daraja la kiwanda kidogo huku akibainisha madhara wanayo tambulika kisheria ni kuwa ni pamoja na vumbi la unga, Moshi na mngurumo wa mashine. 

Aidha Bwana MLAHAGWA amesema “Viwanda ambavyo vipo kwenye makazi ya watu ni hivi vidogo huwa tunasema angalu saa kumi na mbili jioni viwe vimfungwa kwa sababu jioni ni muda wa kupumzika, sasa ikiwa familia inataka kupumzika halafu bado kiwanda kinafanya kazi itakua ni usumbufu”  

MLAHAGWA amewataka wamiliki wa mashine za kusaga na kukoboa zilizopo wilayani Pangani kuzingatia sheria na kufunga mapema mashine hizo ili kuondoa usumbufu kwa wananchi, vinginevyo sheria itachukua mkondo wake.

No comments

Powered by Blogger.