ZAIDI YA KILO SITINI ZA SAMAKI WALIOVULIWA KWA UVUVI HARAMU ZAKAMATWA WILAYANI PAGANI



Zaidi ya kilo sitini (60) za Samaki waliovuliwa kwa uvuvi haramu wa milipuko ya mabomu zimekamatwa wilayani Pangani Mkoani Tanga, kufuatia doria zinazoendelea za kudhibiti shughuli za uvuvi huo Wilayani humo.

Akizungumza na Pangani fm Afisa doria Uvuvi Wilayani Pangani Bwana Jorwam Rebo, amesema kuwa jana wakati akiwa kwenye doria na timu yake wakishirikiana na kamati ya BMU katika kijiji cha Bweni wilayani humo, wamefanikiwa kukamata mzigo ambao baada ya kuukagua wamejiridhisha kwamba ni samaki waliovuliwa kwa milipuko ya mabomu. 

“Na mpaka sasa muhusika tumemfikisha katika vyombo vya dola na taratibu za kisheria zinaendelea” amesema. 

Aidha Bwana Jorwam amesema kuwa pamoja na jitihada ambazo wamekuwa wakizifanya katika kudhibiti uvuvi haramu kwa kushirikiana na vyombo vya dola, kwa kiasi kumekuwa na woga kwa watu kutumia uvuvi haramu ijapokuwa wengi wao wamekuwa wakitekeleza shughuli hizo kwa kujificha. 



“Wilaya zetu za jirani ndo zinachangia kwa kiasi kikubwa shughuli za uvuvi haramu hapa kwetu, kwani hata ukiangalia samaki tuliowakamata, hawa ni wavuvi amabo wametoka kijiji cha mwarongo ambacho kipo halmashauri ya jiji la TANGA, na kwasababu tulikuwa tunawafatilia wametukimbia na kurejea kwao”amesema Bwana Jorwam.

Ameongeza kuwa katika kudhihirisha wao hawako pamoja na watu wa uvuvi haramu na wanaofanya biashara hizo, wataendelea kufanyakazi kila siku hasa katika maeneo yaliyokithiri shughuli za uvuvi haramu Ushongo, Sange, Kipumbwi na Mkwaja.
“Kikazi tumejidhatiti sana, unavyoona tunafanya doria za kushtukiza, tunapata taarifa, tunaenda bila watu kujua na sisi tunajiridhisha tunakamata. Waendelee kutuamini na tuendelee kupeana taarifa tutaifanya kazi” amesema Jorwam.

Shughuli za uvuvi haramu Wilayani Pangani hufanyika kwa ushirikiano kati ya watu kutoka nje ya Pangani na baadhi ndani ya Wilaya, ambapo mpaka sasa jumla ya wavuvi 1570 Wilayani humo wanatambulika kisheria, ukiachilia mbali wengineo wanaoendelea kufanya shughuli hizo kwa njia zisizo rasmi.

No comments

Powered by Blogger.