MHESHIMIWA AWESSO KUANZA ZIARA YA KIKAZI WILAYANI PANGANI KESHO



Naibu waziri wa Maji na Umwagiliaji nchini ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Pangani Mheshimiwa Jumaa Hamidu Aweso kesho anatarajiwa kuanza ziara ya kikazi ya jimboni kwake, kwa lengo la kusikiliza kero za maji na kuzitatua.

Akizungumza na Pangani fm mapema jioni hii katibu msaidizi wa Mbunge wa Jimbo la Pangani Ndugu Salumu Kanyama, amesema Naibu Waziri huyo ambaye ataanza ziara yake Wilayani Pangani hapo kesho tarehe 27 hadi 29 mwezi huu, huku akiwataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika maeneo atakayotembelea.

“Kwa hiyo ataanza kuzungumza na wazee wa Pangani pale katika ukumbi wa halmashauri ya Pangani kuanzia saa nne kamili asubuhi, halafu saa saba mchana atafanya kikao na wakuu wote wa idara ya halmashauri pamoja na wataalamu wote, na kisha jioni atamalizia na mkutano wa hadhara katika eneo la sokoni hapa Pangani  Mjini” alisema Kanyama.

Mbali na kuanza ziara hiyo kesho, lakini pia Naibu Waziri huyo atakuwa na kazi maalumu mkoani Tanga na kisha  ataendelea na ziara yake fupi Wilayani Pangani siku ya Jumapili, pamoja na kwenda kutoa tamko la matumizi sahihi ya kiasi cha shilingi za Kitanzania Milioni 500.8 ambacho kimeshaingizwa katika kijiji cha MTANGO kata ya Ubangaa kwa ajili ya mradi wa Maji.

Katika hatua nyingine Bwana Kanyama ameongeza kuwa kufuatia siku chache za ziara hiyo, amewatoa hofu wananchi wa Pangani kuwa baada ya Naibu waziri wa Maji na Umwagiliaji Muheshimiwa AWESO kumaliza vikao vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, atafanya ziara kubwa katika vijiji vyote vilivyopo wilayani Pangani.

Ziara hii ni ahadi ambayo Naibu waziri wa maji na umwagiliaji nchini ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Pangani Muheshimiwa Jumaa Hamidu Aweso aliitoa kuwa ataifanya baada ya kumaliza ziara yake ya kikazi mkoani SHINYANGA, ambapo ziara hii ataifanya kwa ajili ya kuzungumza na wananchi wa jimbo lake, huku akiambatana na timu yake ya wizara ya maji ili kuja kupanga mikakati ya pamoja katika kutatua changamoto ya maji hususani kwa maeneo ambayo yana shida kubwa ya upatikanai wa huduma hiyo.

No comments

Powered by Blogger.